Header Ads

Wasichana 82 wa Chibok, waachiwa huru na Boko Haram

Ofisi kuu ya Rais wa Nigeria imethibitisha kuwa wanafunzi 82 wa shule ya wasichana wa Chibok, waliotekwa nyara na wanamgambo wa kiislamu wa Boko Haram mnamo mwaka wa 2014, wameachiwa huru.
Maafisa wanasema kuwa waliachiwa huru, kufuatia majadiliano ya muda mrefu na ubadilishanaji washukiwa wa Boko Haram, waliokuwa wamezuiliwa na wakuu wa nchi hiyo.
Wasichana hao ni miongoni mwa zaidi ya wanafunzi wanafunzi 270 waliotekwa nyara kutoka shule ya malazi katika mji wa Chibok ulioko kaskazini mashariki mwa Nigeria.
Wasichana hao wote 82 kwa sasa wanalindwa na jeshi la Nigeria mahali salama, baada ya kuletwa kwa barabara kutoka maeneo ya ndani kabisa vijijini, hadi katika kambi ya jeshi ya Banki, karibu na mpaka na Cameroon, hayo ni kwa mjibu wa mwaandishi habari wa BBC Stephanie Hegarty kutoka Lagos.
Mwaandishi anasema kuwa, familia nyingi huko Chibok wamefurahia taarifa hiyo ya hivi punde lakini wapiganaji hao wa Boko Haram, wangali wakiwazuilia zaidi ya wanafunzi 100.
Ni sehemu ya maelfu ya watu ambao wametekwa nyara na wanamgambo hao, walioanzisha vuguvugu hilo miaka minane iliyopita.
Utekaji nyara huo ambao ulifahamika baadaye kama "Chibok girls" ulisababisha kilio kikubwa kote duniani na kampeini za kutaka waachiwe huru ikatanda kote katika mitandao ya kijamii.
Kabla ya hatua hii ya hivi punde ya kuwaachia wasichana hao, inakisiwa kuwa zaidi ya wasichana 195 wangali hawajulikani waliko.
Idadi ya washukiwa wa Boko Haram ambao wameachiwa huru na utawala wa Nigeria, bado haijajulikana.

Chanzo: BBC

No comments